UMEME WAPANDA BEI ,KUANZA KUTUMIKA MWAKA MPYA ANGALIA HAPA GHARAMA KAMILI - MKWELITZ BLOG

Breaking

.

.

.

.

Saturday, December 31

UMEME WAPANDA BEI ,KUANZA KUTUMIKA MWAKA MPYA ANGALIA HAPA GHARAMA KAMILI










Watanzania  wataanza Mwaka Mpya kwa mabadiliko katika nishati ya umeme, baada ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kuongeza bei ya umeme kwa wastani wa asilimia 8.5.


Mamlaka hiyo imetangaza ongezeko hilo, baada ya kushawishika na sababu za nyongeza kupitia maombi yaliyowasilishwa na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), ambapo imeongeza bei ya umeme kutoka Sh 242.34 hadi 263.02 kwa uniti.

Oktoba 4, mwaka huu Tanesco iliwasilisha ombi la kupandisha gharama za umeme katika mamlaka hiyo kwa asilimia 18.19 kuanzia Januari mwakani ili kupata mapato ya Sh trilioni 1.9.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo, Felix Ngamlagosi alisema pendekezo la Tanesco, lililenga kuongeza bei ya umeme kutoka Sh 242.2 hadi Sh 286.28 kwa uniti. Alifafanua kuwa gharama za kuzalisha umeme ni Sh 155.35 kwa uniti, kusafirisha Sh 23.76 na kusambaza Sh 107.17.

Ngamlagosi alisema miongoni mwa sababu iliyotolewa na shirika hilo ni kutokana na taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini (TMA) ya uwepo wa mvua chache mwaka ujao, hali itakayoathiri upatikanaji wa maji ya kutosha katika mabwawa ya vyanzo vya nishati hiyo.

Alisema kutokana na hatua hiyo shirika hilo, lilifafanua kuwa litatumia zaidi nishati ya gesi na mafuta katika uzalishaji, tofauti na kipindi cha nyuma ambapo mvua zilikuwa nyingi, hali ambayo gharama za uzalishaji zilishuka.

“Pendekezo lao lilikuwa linalenga kuongeza bei ya umeme kutoka wastani wa shilingi 242.2 kwa uniti hadi shilingi 286.28 kwa uniti, sasa tumepunguza katika makundi yote ya wateja, na tumekataa kuongeza gharama ya asilimia tano kwenye kundi la watumiaji wa uniti chini ya 75 kwa mwezi,” alisema Ngamlagosi.

Alisema shirika hilo lilipendekeza kupandisha gharama za umeme ili kufikia mapato ya Sh trilioni 1.9 mwakani, lakini baada ya Bodi ya Ewura kufanya uchambuzi wake iliridhishwa na hoja hizo, lakini haikuona sababu ya kuongeza kwa asilimia 18.19, badala yake ikapunguza hadi wastani wa asilimia 8.5 sawa na mapato ya Sh trilioni 1.6 .

Ngamlagosi alifafanua kuwa kupanda kwa gharama hizo hakutaathiri maeneo mengi, isipokuwa la D1 linalojumuisha wateja wa majumbani wenye matumizi ya wastani wa uniti 75 kwa mwezi. Kwamba matumizi yatakayozidi, yatatozwa kwa bei ya juu ya Sh 350 kwa kila uniti.

Kwa wateja wa kundi la T1 ‘A’ linalohusisha wateja wa matumizi ya kawaida, ambao ni wa majumbani, wafanyabiashara na taa za barabarani, kunaongezeko la asilimia 7.0 kutoka bei iliyopo sasa. Wakati kundi la T1 ‘B’ linalohusisha viwanda vidogo, mabango, minara ya mawasiliano, imeongezeka kwa asilimia 8.4 sawa na Sh 124 kwa uniti.

Kwa wateja walioko katika kundi la T2 linalojumuisha wateja wenye matumizi ya kawaida ya umeme wa volti 400 ambao matumizi yao kwa mwezi ni zaidi ya uniti 7,500 na mahitaji ya umeme hayazidi 500 kVA kwa kipindi cha usoma mita, imeongezeka kwa asilimia 8.8 kutoka bei ya sasa.

Wateja wa kundi la T3 MV waliounganishwa katika msongo wa kati wa umeme, umepanda kwa asilimia 7.5 kutoka kwa bei ya sasa huku walioko katika kundi la T3 HV waliounganishwa katika msongo mkubwa umeongezeka kwa silimia 5.7.

Katika maombi hayo, Tanesco ilibainisha sababu kadhaa ikiwamo kusaidia utekelezaji wa miradi mikubwa mitatu ya upanuzi wa mitambo ya umeme, kuboresha miundombinu ikiwamo nguzo na transfoma na mradi mwingine wa kuboresha mtandao wa kusafirisha na kusambaza nchi nzima.

Aprili mwaka huu, Tanesco ilituma maombi kwa Ewura ya kupunguza gharama za umeme kwa asilimia 1.1, lakini baada ya mamlaka hiyo kupitia maombi hayo, ilipunguza gharama hizo kwa asilimia 1.5 hadi 2.4.
























No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Responsive Ads Here