fedha nyingi za kusanywa tetemeko la Bukoba - MKWELITZ BLOG

Breaking

.

.

.

.

Wednesday, September 14

fedha nyingi za kusanywa tetemeko la Bukoba

Na Mustafa Ismail

Huku  vifo vya waathirika wa tetemeko la ardhi mkoani Kagera vikiongezeka na kufikia 17, uongozi wa mkoa huo umesema zinahitajika zaidi ya Sh bilioni 2.3 kwa ajili ya mahitaji mbalimbali ya waathirika, na tayari serikali jana imehamasisha na kupatikana zaidi ya Sh bilioni 1.4.
Kati ya fedha hizo zilizopatikana, Sh milioni 700 zilikuwa ahadi, fedha taslimu Sh milioni 646, Dola za Marekani 10,000, Euro 10,000 na mifuko 2,800 ya saruji.
Kampuni za mafuta ya Oilcom, GBP na Moil, zimejitolea kujenga shule mbili za sekondari zilizoathiriwa na tetemeko hilo. Shule hizo zimefungwa. Jumamosi iliyopita, saa 9.27 alasiri mji wa Bukoba ulikumbwa na tetemeko la ardhi, ambalo nguvu ya mtetemo wake ulikuwa ni 5.7 kwa kutumia skeli ya “Ritcher”.
Ukubwa huo ni wa juu kiasi cha kuleta madhara makubwa ikiwemo kuanguka nyumba, nyingine zimepata nyufa, watu 17 wamekufa, na mamia wawamejeruhiwa.
Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Salum Kijuu alisema, baada ya Kamati ya Maafa ya Mkoa na Kamati ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama, wamefanya tathmini ya haraka na kubaini mahitaji kwa wananchi walioathirika.
Alitaja mahitaji ya muhimu ambayo yanahitaji kwa haraka ni dawa, tiba na vifaa tiba, vifaa vya ujenzi mabati 90,000 yenye gharama ya Sh bilioni 1.7, saruji mifuko 9,000 yenye thamani ya Sh milioni 162, mbao zenye thamani ya Sh milioni 450 na misumari yenye thamani ya Sh milioni 12 ambapo jumla ni Sh bilioni 2.3. Majaliwa achangisha bil 1.4/- Wakati Kijuu akisema hayo, Majaliwa amehamasisha wafanyabiashara pamoja na mabalozi, kuchangia na kuchangisha zaidi ya Sh bilioni 1.4.
Katika hafla fupi iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam, Waziri Mkuu Majaliwa alieleza kuwa kutokana na tetemeko hilo kubwa, imelazimu serikali kuzifunga shule mbili za sekondari zilizoharibiwa vibaya za Nyakato na Ihungo. Waziri Mkuu alisema tetemeko hilo ni kubwa ambalo halijawahi kutokea nchini, hivyo haikutarajiwa na wala hakukuwa na maandalizi ya kukabiliana na hali kama hiyo.
Alisema mpaka jana watu 17 walikuwa wamefariki dunia huku 253 wakijeruhiwa na 145 walikuwa wako katika hospitali huku vitu vingi pamoja na miundombinu vikiharibika.
Katika miundombinu ya shule nne za Nyakato, Ihungo, Kashenge na Buhembe, zimeharibika ikiwemo vyoo, nyumba za walimu, kumbi za shule na mabweni yameharibika kabisa pamoja na hospitali na vituo vya afya navyo vimeharibika.
Alisema kuna baadhi ya sehemu hali ni mbaya na wanahitaji msaada ambapo nyumba 840 zimeanguka kabisa chini huku nyumba na majengo 1,264 yakiwa na nyufa na kamati ya maafa katika mkoa pamoja na viongozi wake wanaendelea kufanya tathmini ya kiasi cha hasara iliyopatikana.
Alisema serikali imefanya juhudi katika kukwamua maisha ya wananchi wake na mawaziri watatu wako mkoani humo kuangalia namna ya kukabiliana na majanga hayo ambao ni Waziri wa Ujenzi, Profesa Makame Mbarawa, Elimu Profesa Joyce Ndalichako na Waziri wa Nchi katika ofisi yake, Jenista Mhagama.
Alisema kupitia kitengo cha maafa katika Ofisi ya Waziri Mkuu wamefungua akaunti hiyo katika benki ya CRDB huku wakiendelea na maandalizi ya kupata namba za kuchangia kwa simu ya mkononi huku akiwashukuru wabunge walioamua kuchangia maafa hayo kwa kutochukua posho zao za siku ya jana.
Mabalozi, Wafanyabiashara Mkuu wa Jumuiya ya Mabalozi, Balozi wa Zimbabwe nchini, Edzai Chimonyo alisema kutokana na tarifa hiyo kuwa ya ghafla na wako sehemu mbalimbali duniani watakusanyika na kuwasilisha michango yao. Lakini, hata hivyo, balozi mbalimbali zilijitokeza kuwasilisha michango yao ikiwemo Ubalozi wa China, uliotoa Sh milioni 100, wafanyabiashara wa Kichina walitoa Sh milioni 100 na Ubalozi wa Kuwait Sh milioni 50.
Pia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ilitoa mchango wa wafanyakazi wake Sh milioni 10 huku ikiandaa matembezi ya kuchangisha fedha zaidi kwa waathirika wa tetemeko hilo yatakayofanyika Jumamosi wiki hii. Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dk Azizi Mlima alisema wameanza kwa kukabidhi fedha hizo ambazo ni mchango wa wafanyakazi, lakini Jumamosi wamealika wadau mbalimbali katika matembezi hayo watakayochangia zaidi.
Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Reginald Mengi alisema wafanyabiashara wako pamoja katika kuhakikisha wanakabiliana na tatizo hilo na kuipongeza serikali kwa hatua za haraka walizochukua kukabili majanga hayo.
Mengi alichangia Sh milioni 110, Kampuni ya Mohammed Enterprises (MeTL) kupitia kwa Ofisa Mtendaji Mkuu wake, Mohamed Dewji ilitoa Sh milioni 100, Kampuni ya Bia (TBL) Sh milioni 100, Chama cha Wauzaji Mafuta kwa Rejareja Sh milioni 250 huku Umoja wa Waagizaji Mafuta ukiahidi kuchangia baada ya kikao watakachokaa leo.
Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage alishukuru kwa wafanyabiashara na mabalozi kwa michango hiyo na kuomba ipatikane kwa haraka ili kusaidia wananchi wa mkoa huo kurejea katika maisha yao ya kawaida.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Responsive Ads Here