Na Mustafa Ismail
RAIS John Magufuli ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taifa wa
Chama Cha Mapinduzi (CCM), amefanya ziara ya kushitukiza katika ofisi za gazeti
la Uhuru, mali ya chama hicho tawala na kuagiza ndani ya mwezi huu, wafanyakazi
walipwe mishahara yao wanayodai inayofikia Sh milioni 609.
Aidha, ameagiza kupatiwa orodha ya taasisi za serikali
zinazodaiwa na Magazeti ya Uhuru na Mzalendo, na pia ameagiza deni linalodaiwa
na Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) kutokana na kutowasilishwa kwa
makato ya wafanyakazi lilipwe.
Katika mazungumzo yake na wafanyakazi kwenye ofisi hizo
zilizopo Mtaa wa Lumumba jijini Dar es Salaam, wafanyakazi wamelalamikia
kutolipwa mishahara yao kwa miezi saba, kutotolewa kwa michango ya wafanyakazi
kwa NSSF, kuuzwa kwa mtambo wa kuchapisha magazeti katika hali ya kutatanisha,
kutotambuliwa katika ajira kwa baadhi ya wafanyakazi, kutolipwa kwa madeni
wanayozidai taasisi za Serikali na wanaostaafu kutolipwa mafao yao.
Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu, wafanyakazi hao pia
wamemueleza Dk Magufuli kuwa Bodi na Menejimenti ya Kampuni ya vyombo vya
habari vya chama inayoendesha gazeti la Uhuru na Redio Uhuru, zimeshindwa
kuendesha vyombo hivyo na wamemuomba aingilie kati ili kuvinusuru, ambavyo kwa
sasa vina hali mbaya kutokana na kukabiliwa na madeni makubwa, na biashara yake
imeshuka kwa kiasi kikubwa.
Akijibu malalamiko hayo, Rais Magufuli aliyetembelea ofisi
za Uhuru akitokea ofisini kwake katika jengo la Makao Makuu ya CCM Ofisi Ndogo
Lumumba, amemuagiza Katibu Mkuu wa CCM,
Abdulrahman Kinana kuhakikisha mishahara yote wanayodai
wafanyakazi inayofikia Sh milioni 609, inalipwa ndani ya mwezi huu wa tisa,
ameagiza kupatiwa orodha ya taasisi za serikali zinazodaiwa na magazeti ya
Uhuru na Mzalendo, na ameagiza deni linalodaiwa na NSSF kutokana na kutowasilishwa
kwa makato ya wafanyakazi lilipwe.
Kuhusu malalamiko dhidi ya Bodi na Menejimenti ya kampuni
hiyo, ajira za wafanyakazi, mafao kwa wastaafu, kuuzwa kwa mtambo wa kuchapisha
magazeti na mazingira magumu ya kazi, Dk Magufuli ameahidi kuyafanyia kazi.
Aidha, Dk Magufuli aliwapongeza wafanyakazi wa gazeti la
Uhuru kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya licha ya kukabiliwa na changamoto
kubwa na amewahakikishia kuwa anatambua umuhimu wao na kwamba atahakikishia
anaboresha hali ya chombo hicho muhimu.
Wakati huo huo, Rais Magufuli amemjulia hali Spika mstaafu
wa Bunge, Samuel Sitta ambaye anaendelea kupata matibabu jijini Dar es Salaam
na hali yake inaendelea vizuri.
chanzo Habari leo
No comments:
Post a Comment